Wednesday 27 September 2017

SIKUKUSUDIA ILA KWA SASA NI MAREHEMU.

Katika huzuni twaomboleza, katika huruma tumefarijiwa sisi tuliyofiwa. Tuko makuburini ambapo kanisa, ndugu na jamaa wameungana nasi ili kumpa mkono wa buriani mamangu. Namshukuru Mungu kwa kumpumzisha kwani aliteseka sana nyakati zake za mwisho. Aliugua saratani kwa muda mrefu na kuugua kwake kuliniathiri pakubwa. Hata ingawa namshukuru Mungu kwa kumpumzisha, binafsi nimebaki na upweke. Nilimzoea sana na ndiye aliyekuwa rafiki wangu wa karibu. Natafakari maisha yatakavyokuwa bila yeye na wazo la babangu linanipa kichaa! "Hivi Mungu mbona ukamsahau na huyu mzee?" Najiuliza! Mazishi yalikamilika vizuri, watu wakatawanyika nami nikarejea nyumbani.

Ni wakati wa jioni nami sina hamu ya kufanya chochote kile. Naelekea katika chumba changu cha kulala ili angalau nipumzishe akili. Kifo cha mamangu kilikuwa pigo kubwa kwangu Ila kwa upande mwingine ulinipa fursa ya kujitaftia uhuru. Uhuru ambao sharti ningeupigania, ili kujinasua kutoka kwenye minyororo ya utumwa. Ni mengi nimeyapitia mikononi mwa babangu mzazi, na kila nikiwaza machozi hunitiririka.

Babangu ni mmoja wa waumini tajika kijijini, tena mwenye sifa kemkem. Anapendwa na wengi na ni wa kuheshimika, ila kwangu mimi, ni mbweha aliyevalia ngozi ya kondoo au nimuite ibilisi mtu. Babangu alinidhalilisha na kunigeuza kijakazi, si wa kazi za nyumbani bali wa kumtimizia haja zake za kimapenzi. Alimtishia mamangu na kumlazimisha kunishawishi ili nikubali matakwa yake, kwani mamangu hakuwa na uwezo wa kumtosheleza kutokana na hali yake ya kiafya. " Mwanangu hatuna la ziada, tena katika hali yangu tutaishi vipi bila babako? Naomba umtimizie iwapo unanipenda na unataka uzidi kuniona hai. Naelewa uzito wa jambo hili ila itakuwa siri" Alinisihi mamangu.

Nilimchukia babangu, "hivi huyu ni babangu mzazi kweli?" Nilishindwa kuelewa. Mbona asingetafta mke mwingine? Au ndio kuikuza heshima yake na kuoneka mungwana? Maisha yalikuwa magumu, kumwona mamangu akiteseka na ugonjwa huku babangu akinilawiti kila uchao, bora nife! Nilishindwa kujidhibiti huku maisha yangu ikikosa mwelekeo. Niliathirika pakubwa hasa kisaikolojia, adhabu ilioje!

Usingizi ulinijia na kwa ghafla nikashtushwa na sauti ya babangu. "Mbona mapema leo mwanangu?" Sauti yake yenye uzito iliniamsha. Ni vipi nilisahau kuubana mlango? Sikuwa tayari kabisa kuzidi kumhudumia. Tena mamangu ndio kafa, hivi nimtimizie kwa nini? La! Ni sharti nitie kikomo. "Hivi tumebaki wawili tu, mbona usigure na kuungana nami kwenye chumba changu?" Alizidi kunieleza. Maneno Haya niliyaona ya utani. Hivi huyu mzee ana akili timamu? Mamangu kazikwa leo tu, na mchangani hajamaliza hata siku, naambiwa nikaridhi chumba chake? Kweli dunia ina mambo.

Sikutaka kuzidi kumskiza kwani alinikera, wala sikuwa tayari kumtimizia matakwa yake, hivyo nikamwomba aondoke. Alisusia na kunivuta kwa nguvu ili niandamane naye. "Nimevumilia ya kutosha! Naomba uniache tena niko radhi nikuondokee hata sasa!" Nilipayuka huku nikijaribu kujinasua kutoka mikononi mwake. Alinizidi nguvu na hatimaye akanirusha kitandani kwake. "Ntaishi hivi mpaka lini? Mungu naomba unipiganie." Nilijiambia kimoyomoyo, ni kweli mnyonge hana haki.

Alijaribu kunishika kwa nguvu nami nikakataa abadan katan kushikamana, ikawa ni vita dhidi ya baba na bintiye kisa mapenzi. Nilinyoosha mkono wangu kwa kutafta kifaa chochote kitakachonisaidia na kwa bahati nzuri nikahisi kifaa chini ya mto. Sikusita kulichomoa ili nijizuie ila nilishtuka kuona kuwa ilikuwa bastola. Alijaribu kunipokonya nami nikajitahidi kulistahimili na katika ile harakati, sijui aliyeibonyeza ni nani, kwani nliskia mlipuko na babangu akawa anavuja damu nyingi ajabu. Lo! Ndio kafa!

Sikujua pa kuanzia, nilichukuwa simu yake ya mkono na kubonyeza nambari ya dharura ili kuwaita polisi. Niliwaeleza kuwa babangu ameaga katika hali ya kutatanisha na wakanihakikishia kuwa watafika kwa takriban muda wa nusu saa. Niliutazama mwili wa babangu kwa majonzi, nilimchukia ndiyo lakini sikunuia kumkatizia maisha yake. Nilipigania uhuru wangu lakini sikutarajia kuvuja damu. Hivi nitawaeleza nini polisi? Ni nani atakayeamini maneno yangu, kuwa babangu alikuwa ananidhulumu kimapenzi na katika hali ya kujiokoa haya yakatokea?

Walitimiza ahadi yao na baada ya nusu saa waliwasili. Walikuwa watano, wanaume wanne na mwanamke mmoja, nami nikawaelekeza hadi chumbani. "Hivi ni nini kilitokea?" Mmoja wao aliuliza. "Ni..liku..wa.....nnaa..ja.ri..bu.." nilishindwa kujieleza nikaishia kwa kilio. Waliukagua mwili na kubaini kuwa alikufa kwa risasi. Ushahidi ulikuwa wazi kuwa hakuna aliyetuvamia na ni mimi ndiye mshukiwa pekee. Niliandamana nao hadi kituo cha polisi, huku mwili wa babangu ukipelekwa katika chumba cha kuhifadhi maiti.

"Msichana mbona ulimuua babako?" Maswali yalizidi, "na bastola ulitoa wapi? Una ruhusa ya kuimiliki?". Yote haya nilijibu kwa kimya, chambilecho wahenga, kimya kingi kina mshindo mkuu. Nilishindwa kabisa kujieleza kwani wengi walimjua babangu kinyume na nilivyomjua mimi. Mamangu pekee ndiye angekuwa wa kuniokoa lakini hayupo tena. Hakukuwa na kesi ya kuskizwa kwani ilikuwa dhahiri kuwa nilimuua babangu, na jela ikawa inanikodolea macho.

Pengine huu ndio uhuru niliotamania, pengine haya ndiyo maisha yatakayonifaa, maisha bila babangu, maisha bila kulawitiwa, maisha gerezani.
picha imedhaminiwa na google.

Tuesday 26 September 2017

MAJUTO NI MJUKUU

 Azizi Ni kipusa aliyezaliwa na kulelewa kwa njia ya kipekee. Binti huyu mwenye maumbile ya kupendeza na sura nzuri alivutia wengi, wa karibu na mbali, kwenye vitongoji hadi vijiji, wazee kwa vijana, bila shaka alikuwa mfano bora wa binadamu aliyeumbwa akaumbika. Pasi na sura, Azizi alikuwa binti mwenye hulka njema, wengi walimsifia kwa heshima aliyokuwa nayo kwa waliomzidi umri, shuleni alipendwa na walimu, kwani kwenye buku hakuachwa nyuma. Alikua miongoni mwa wanafunzi bora na kila muhula alitunukiwa zawadi chungu furika, ama kweli, Chanda chema huvikwa Pete na mcheza kwao hutuzwa.

Kadri siku zilivyozidi, Azizi naye maisha yake yalianza kubadilika. Alimaliza shule ya upili na kufuzu kwa alama nzuri tu, hivyo akajipa nafasi ya kujiunga na chuo kikuu. Hapo ndipo maisha yake yalianza kufuata mkondo usioeleweka! Au ndio kitumbua kiliingia mchanga? Na kidagaa kumuozea?

Azizi alikuwa si yule Azizi tuliyemjua! Alibadilika na kuwa asiyeambilika wala kusemezeka, hakuskia la mwadhini wala mteka maji msikitini. Wazazi wake walimsikitikia, walimsihi asijekuiga ya dunia na kusahau alikotoka. Walimwonya dhidi ya maisha ya anasa na vijana waso na maana. "Mwanangu chunga, maisha ya ujana yasije yakakuangamiza" Babake alimwonya, ila haya yote yaliangukia sikio la kufa lisilosikia dawa, ama tusema sikio la Azizi alilitia nta kwani yaliingilia kulia na kutokea kushoto.

Ulimwengu ulimkodolea macho kodo! Ulimwita na kumdekeza kwa sana, laiti angalijua masaibu yatakayomkuta! Maskini Azizi! Alijiona kesha fika, mtindo wake wa mavazi ulibadilika, bui bui na mitandio aliyaona ya kishamba na kuwa mwacha mila. Alivaa vijinguo vya kumbana, si vipaipu si mgongo wazi si mini sketi! Binti wa kidijitali! Viatu vya kumuinua juu juu sijui ndio "mkodo mkodo". Alijirembua na kujipodoa kama malkia, hata kipofu angemnusia na kumtamania. Biashara matangazo, naye alijitangaza si haba, kumbuka chema chajiuza, ila yeye aliamua kuwa kibaya cha kujitembeza. Lo! Kaharibikia ukubwani.


"Mwanangu nakupeleka shuleni ukasome. Vyuo vikuu vina majaribio mengi, huko kuna aina zote za raha na karaha, nakuomba uepuke yasokufaa", mama Azizi alimdokezea huku akimdara begani. " I know mum, I'll be fine!" Alijibu Azizi huku macho ameyalegeza kwa mamake. Mamake alimhurumia kwani alikua ameanza kumea pembe tayari, ila aliomba maji yasije yakazidi unga. Alimpeleka mwanawe shuleni na kubaki akimwombea mema huku akiwa na matumaini kuwa mwanawe atazidi kufanya vizuri kwani kwake kupita mitihani Ilikuwa ni sheria kama ibada.



Kama ilivyo ada ya vyuo, wanafunzi wa kike wa mwaka wa kwanza huwa kama ua linalonawiri shambani. Wanafunzi wa kiume hasa wale wenye ufisi huwamezea mate na kuwatamania kutokana na ubichi wao na hivyo huwashambulia na kuwatongoza kwa udi na uvumba, na hapa ndipo wengi hutegwa wakateguka.

Mandhari mapya, maisha mapya na hakuna wakukufwatilizia uko wapi? wafanya nini? na nani? Uhuru ulioje! Maisha hapa ni tofauti kabisa, kudurusu vitabu na kufanya kazi za ziada ni kwa hiari yako. Ni juhudi za mwanafunzi mwenyewe kutumia akili kufanya jambo linalofaa kwa wa wakati unaofaa, kwani hata ingawa wanafunzi wana uhuru huu, mwishowe haya yote huangaziwa ili kumpa mwanafunzi jumla ya alama, mwisho wa semesta, na hapa ndipo wengi hufeli!

Kwa binti Azizi, haya ndiyo maisha aliyoyatamania, maisha bila ratiba. Kufanya unachokitaka bila kunyoshewa kidole wala kelele za mamake za mara kwa mara, raha ilioje! Azizi alijisahau kabisa kama alikua mwanafunzi aliyepelekwa shuleni kusoma, kwake yeye ni kama alikuwa likizo fulani kujistarehesha. Masomo yaligeuka raha iliyokithiri mipaka.

Alijiunga na kundi la wasichana ambao pia waliipa raha kipaumbele. Wote hawa walipoteza mwelekeo wa maisha huku nia yao kuu ikiwa kuutetemesha mtandao na mitindo ya kimavazi, urembo wao na jinsi wanavyojua kuponda raha, yaani "kuparty". Walipiga picha ya kila aina na kuyajaza kwenye akaunti zao za "Facebook" na "Instagram". Waliishi kwa kulewa huku wazazi wao wakidhania kuwa wana wao wako shuleni, na wanasoma kwa manufaa yao ya baadaye, kumbe ndivyo sivyo.

Mapenzi ni kizungu zungu, mapenzi yanaezakufanya ukachanganyikiwa usijue la kufanya. Ni vigumu kutofautisha mapenzi ya dhati na ya ulaghai, ila kwa wengi bora mapenzi, ilimradi moyo umeridhika. Lakini je, ina maana kuwa wana wetu wa vyuo wanafahamu fika maana ya mapenzi? Azizi na kikundi chake walitamaniwa na wengi na katika harakati ya kusumbuliwa na vijana hapa na pale, bila shaka alijikuta kwenye boksi ya Kingi.
Kingi, kijana mtanashati na aliyeunga misuli kama mnyanyua vyuma, aliwazingua mabinti wengi, ila kwa Azizi alifika. Mapenzi yalinoga kwa kiasi cha kumshawishi Azizi kugura kwenye vyumba vya wanafunzi shuleni ili waishi pamoja kwenye chumba cha kukodisha kama mke na mume, haya kama si ya Musa nitayaita ya firauni!




"Beb uko na class leo?"
"Niko na class, but sijiskii kuenda."
Haya ndiyo yalikuwa mazungumzo kati ya hawa wapenzi wawili waliojisahau kuwa ni wanafunzi. Mara nyingi walikuwa wavivu wa kwenda darasani. Walitumia simu zao za rununu kuwasiliana na waliohudhuria masomo ili kujua mambo yalivyokua yakiendelea darasani. Siku ziliyoyoma mtindo ukiwa ni huu huu. Mapenzi yalizidi kunoga, wakala raha zao na pasi kujua, Kingi alifunga bao!

"Mja mzito?" Alimaka mwana wa watu. Hii ni baada ya kujihisi mgonjwa na kujipeleka kwenye zahanati ya shule. Alilazimika kupimwa magonjwa mengi ila uja uzito hakuutarajia kabisa. Nguvu zilimwishia akajiketisha kitako asijuwe pa kuanzia. "Nurse uko sure?" Alimuuliza muuguzi, huku sauti yake ikiwa yenye huzuni tele. Alimwona mamake akiwa amesimama mbele yake, ".....Nakuomba uepuke yasokufaa" aliyakumbuka maneno ya mamake, huku machozi yakimtiririka njia mbili mbili. Alinyanyuka na kujikokota kuelekea chumbani kwao, ili amwelezee mwenzako yaliyowakumba.

Kingi aliipokea habari kwa mshtuko! Alimpenda Azizi ila hakuwa tayari kuitwa baba, la! Suluhisho ni lipi? Yalikuwa yashamwagika na hayangezoleka. Wawili hawa walitofautiana, kwani Kingi alitaka Azizi akaavye mimba lakini yeye hakuwa tayari. Walikorofishana kwa muda huku kila mmoja akimnyooshea mwenzake kidole cha lawama. Kwa kutokubaliana, Azizi alifungasha virago vyake na kumuondokea Kingi. Msururo wa maswali ulimjaa akilini akose wa kumjibu. Alitamani dunia ipasuke na kummeza mzima mzima, kwani alijihisi si wa maana tena.

Azizi alijikuta katika hali ngumu mno. Mitihani ilikaribia, marafiki walimtenga na wazo la kuwa mama mtarajiwa lilikuwa kama jinamizi. Aligeuka na kuwa gumzo la wengi pale shuleni. Waliyomwonea gere walimsimanga huku wengine wakimuonea huruma. Mwana wa watu alinyong'onyea, alitamana yote haya yawe ni ndoto, na kuwa ataamka na kurudia maisha yake ya zamani. Alitamana miujiza ifanyike, wakati urudi nyuma ili arekebishe alipokesea, lakini ng'o! aliangulia pang'anda. Lisilo budi hubidi, Naye hakuwa na budi ila kukubali yaliyomfika.

Kutokana na kutohudhuria kwake kwa masomo, Azizi hakuweza kujiandaa vilivyo kwa mitihani. Aliamua liwe liwalo, na kukosa kufanya mtihani huo. Alikuwa ashateleza na kwake yeye ule uja uzito ulimpa stresi zaidi ya chochote kile. Mitihani ilikamilika na wakati wa likizo ukawa umetimia. Hakutamani kabisa kwenda nyumbani, kwani babake ni simba, tena mwenye ghadhabu ajabu. "Hivi nitaenda kwa nani? Nitamweleza nini babangu?" Aliwaza.


Monday 25 September 2017

MOYO WANGU NAKUPA KAMA ZAWADI

"Sabrina! Sabrina! Fungua tafadhali! Mwanangu fungua tuyazungumzie." Babangu anayakatisha mawazo yangu huku akiubisha mlango kwa fujo na kujaribu kuufunga. "La baba, siwezi! Sitaki! Naomba uniache. Sitaki kumwona mtu yeyote kwa sasa." Nanyanyuka kitandani na kuelekea katika roshani ya chumba changu kilicho katika orofa ya nne. Moyo wangu unapiga kwa kasi huku nikiwa na hisia za kujirusha toka pale ghorofani na kujitoa uhai ili kutia kikomo machungu ninayoyapitia. Mawazo yanazidi kunikera na kunikereketa maini, hasa nikilitazama gauni langu nililovua na kutupa pale sakafuni. "Hivi Aly yuko wapi? Kuna uwezekano kuwa katekwa nyara? " Maswali hayaishi akilini. Nachukuwa simu yangu kutizama kama ametuma angalau hata ujumbe kunieleza aliko. La hasha! Sina ujumbe wowote, tena la kunitonesha kidonda zaidi ni kuwa simu yake ni mteja. Hivi ni nani kanipokonya tonge langu mdomoni?

Siku ilianza kwa furaha tele, furaha iliyozidi ya tasa aliyejaliwa mwana, leo ni siku iliyotarajiwa kuwa swadakta! Tulirauka che mbichi hata kabla ya jimbi wa kwanza kuwika. Pilka pilka za hapa na pale zilizidi huku simu zikipigwa kila pembe ili kuhakisha kuwa kila kitu kinaenda sambamba jinsi ilivyotarajiwa. Mimi na wasimamizi wangu tulikuwa katika hoteli moja maarafu jijini. Mila na tamaduni zinamkashifu mume kumwona mkewe kabla ya harusi na hivyo  tulizitia maanani. Hata ingawa nilikuwa na furaha ajabu, moyoni nilijawa na uoga huku nikiomba siku yangu iwe ya kufana, wanavyotarajia bi harusi wengi. Ndoto yangu ilikuwa imetimia kwani siku iliyokuwa imesubiriwa kwa hamu na ghamu bila shaka ilikuwa imewadia. Siku yangu ya kuipa kisogo maisha ya uwana wali na kuwa mke wa mtu. Mke wa Aly, mume niliyempenda na kumwenzi kwa sana, kwa dhiki na faraja, kwa hali na mali, kwake nilifika.

Hakuna zuri likosalo dosari na kila adinasi ana udhaifu wake. Kipenzi niliyemchagua hakuwa tofauti na binadamu yeyote yule, ila sijui ni kwa nini babangu mzazi hakumpenda. Babangu ni moja wapo wa wanabiashara mashuhuri nchini na kwa hivyo ni wazi kama mchana kuwa ana utajiri mkubwa. Sina ubainifu wa hakika ni kwa nini hakumpenda Aly, ila kupitia kwa mazungumzo ya mara kwa mara, nadhani alimwona mwenye kitengo cha chini. "Ulimpendea nini lakini? Hivi huyu ataweza kukutunza jinsi ninayokutunza mimi babako?" Aliuliza mara nyingi, kila tulipomzungumzia Aly. Alijaribu kunishawishi kuvunja mahusiano yetu ila juhudi zake ziligonga mwamba.

"Harusi tunayo hatuna?" Sauti zilisikika hewani pindi tu nilipofikishwa kanisani. Shangwe na nderemo zilijaa huku viuno vikinenguliwa. Kanisa ilifurika watu wengi ajabu kupita kiasi cha matarajio yangu. Uoga ulinizidi huku moyo ukinidunda. Babangu alikuja kunilaki, "umependeza mwanangu!" Aliniambia.
Mandhari ya kanisani yalipendeza kutokana na maridadi ya vibofu na maua ya rangi ya manjano na nyeupe, ama kwa hakika palipambwa pakapambika. Rangi hizo ziliwiana na nguo walizovaa wasimamizi wangu, nami nilemetameta ndani ya gauni langu jeupe kama theluji.


Tulitarajia kumpata bwana harusi na wasimamizi wake wawe wamewasili pale kanisani lakini mambo yakawa kinyume, hivyo tukalazimika kuwasubiri.Muda ulizidi kuyoyoma nami nikajawa na wasiwasi. Minong'ono ilikolea huku hali ya sintofahamu ikishuhudiwa. Msimamizi wangu alilazimika kupiga simu ili kubaini ni kipi kilichojiri na hata kabla ya kubonyeza "ok" gari lao liliwadia, "waaahh...angalau" nilishusha pumzi.

Nilipigwa na butwaa wasimamizi waliposhuka na kueleza kuwa hawajui Aly aliko. "Aliji.execuze kwenda ku.recieve call flani, na ndio hakurudi." Alisema mmoja wa wasimamizi wake. "Atiii??!!" Sikuyaamini masikio yangu. Sielewi nilivyovua viatu na kuchomoka mbio kutoka pale kanisani, wala sijui hisia na matukio yaliyofwatia. Kioja cha kusikitisha. Sijui Mambo yalivyokwenda ila nilijikuta chumbani kwangu.

Usaliti ulioje? Mbona leo? Ni heri angeniambia mapema. Nashindwa kuelewa kiini cha Aly kuniacha kwenye mataa. Mbona kanipofua? Je, babangu anaweza kuwa mhusika? Sidhani kwani hata ingawa hakumpenda Aly, aligharamika kwa sana kuifanikisha siku ya leo. Nashindwa kuelewa kabisa, ama kwa hakika, jambo usilolijua ni usiku wa kiza.

 Nilimpenda sana Aly na kwa sasa sihisi kama ntapenda tena. Nilijitolea kimwili, kiakili na kivyovyote vile kuwa naye, ila ni kama sikupangiwa, mipango ya Mtrehemezi hakuna anayeweza kupangua. Labda nitajikaza ili niishi kwa taswira ya muda tuliyokuwa nao, maana kwa sasa najihisi mpweke. Nitabaki na machungu na vidonda vya mapenzi kwani kokote aliko Aly, moyo wangu ameunyofua.

Sunday 24 September 2017

MUIGE MARAGA.

Jasmini kipenzi changu, waraka huu Ni wako

Chenille mwana wa kwangu, nisikize mi ninako

Maisha haya ya tangu, jadi zile za Obakoo

 Mwanangu unapokua, na umuige Maraga.



Ndiye jaji wetu Kenya, Yule mwenye historia

Kazi nzuri alifanya, kila mja kasifia

Wale wezi wa kunyonya, Kura zetu kaangazia

Mwanangu unapokua, na umuige Maraga.



Nina mengi ya kusema, ila nianzie wapi?

Viongozi waso wema, ila tutaenda wapi?

Nchi yetu uhasama, jamani twaelekeapi?

Mwanagu unapokua, na umuige Maraga



Mwana pendo na Moraa, kafa kisa uchaguzi

Mapolisi kwa vifaa, wakaleta uchafuzi

Wakenya bila manufaa, twasubiri uchunguzi

Mwanangu unapokua, na umuige Maraga.



Adhis, Nyash na Kadima, wenye wana Kama
mie
Sisi sote kina mama, wenye wana tuangazie

Kuwalea hima hima, kesha kua wajulie

Ili wanapokua, na wamuige Maraga.


Kadi tama Sina budi, mwisho wangu wa waraka

Mwana uwe mwenye udi, nami naomba baraka

Zidi kuwa na juhudi, maisha siwe dhihaka

Mwanangu unapokua, na umuige Maraga.


Jaji mkuu wa Kenya, David Maraga.

LULU HASSAN

Siulize Ni kwa Nini, Nam enzi huyu Lulu Ueledi wake Shani, taka iga nifaulu Kwenye lugha namba wani, uliza hadi ikulu Mwanahabari shupavu...